Thursday 2 July 2015

Hatua 6 za Kuwalea Viongozi Watarajiwa (Chipukizi)

Habari na karibu ndugu mpenzi msomaji wa blogu hii. Ni matumaini yetu umekuwa na wiki ya mafanikio sana. Ni dhahiri umekuwa ukipata mlo kamili wa akili siku hadi siku kupitia blogu hii. Ninachopenda kukuhamasisha jitahidi katika kila makala inayowekwa hapa tafuta vitu vichache ambavyo vitafanya tofauti kubwa inayoweza kuonekana waziwazi au inayoweza kupimika katika maisha yako na vitu hivo viwe ni rahisi kuanza na kuendelea navyo kadiri unavyosafiri katika safari yako ya kuelekea mafanikio.

Leo nitazungumzia namna ya kuwalea watu wenye sifa za uongozi ambao umewatambua upo nao katika timu yako katika taasisi, ambapo nitakuwa pamoja nawe kukupitisha katika hatua sita za muhimu.


Kwanza, ili kuwa na viongozi wazuri unahitaji kuwapa muda; ukiwa kama kiongozi ambaye unaandaa viongozi watarajiwa unahitaji kuwaamini wale unaowaandaa kwa kuwatamkia wazi wazi na kuwatia moyo namna ambavyo unaamini katika uwezo wao wa kutenda mambo wanayoyafanya na hii itaanza kuwahamasisha na kuwafanya pia wajiamini binafsi. Unahitaji kujitolea ukiwa unamaanisha na kuwepo kwa muda watakaohitaji uwashauri.

Pili, kuwa na msimamo thabiti, bila kujali hali inayojitokeza unahitajika kuwaonyesha msimamo wako  ambao hauyumbishwi na unakuwa katika kiwango kile kile kila mara katika utoaji ushauri, kujitolea muda wako na kuwahamisha. Hii itawasaidia kujenga uaminifu au kukuamini wewe.

Tatu, tambua kufanikisha kwao, waonyeshe kile wanachofanya kina umuhimu na thamani kwako wewe kama kiongozi wao na pia kwa taasisi.Namna rahisi ambayo unaweza kuongeza umuhimu katika kazi wanayofanya hawa unaowaandaa kuwa viongozi ni kuwahusisha kuwa sehemu ya kitu cha thamani kwa kuwapa picha kubwa ambayo taasisi husika imekusudia kuifikia na namna gani wao ni sehemu muhimu ya kufanikisha hilo kufanikiwa.

Nne, wapatie usalama, watu wakifahamu kuwa wapo sehemu salama ni rahisi kuwa na utayari wa kukua, kujiendeleza kwa kujifunza, na hata kuchukua hatari kwa ajili ya kujiboresha wao wenyewe.

Tano, toa tuzo kwa ufanikishaji wa jambo lolote, unahitaji kuwafanya wajue nini matarajio yako na ni tuzo gani watapata au zinawasubiri kwa wao kufanikiwa kufikia au kuzidi matarajiao yako hii itawafanya wajitume kufikia hayo matarajio uliyoyaweka. Na ni vizuri kuhakikisha wanapewa tuzo stahiki ambazo zifanyike kwa njia ya wazi kutegemeana na taratibu mlizoziweka na si lazima ziwe ni za kifedha tuu bali zinaweza kuwa za kutambua mchango wa watu husika katika kufanikisha jambo katika taasisi. Kwa kuwapatia tuzo kwa kazi nzuri iliyofanywa itawasadia kujisukuma kufanya vizuri zaidi.


Sita, wapatie msaada au waunge mkono, hakuna kitu ambacho kinaumiza kama kuwapa watu kazi waifanye na huwapatii msaada wanaostahili na rasilimali wanazozihitaji ili kufanikisha kazi uliyowapa. Tengeneza mfumo mzuri wa wao kupata msaada kutoka kwako na msaada unaweza kuwa ni wa kuwahamasisha, kuwajali, kifedha, kiujuzi, mafunzo au hata kifaa sahihi cha kuwarahishia kazi au mtu wa kuwaongezea nguvu. 

0 comments:

Post a Comment